"*" indicates required fields

If you would like to talk to someone about living with Jesus as your ruler, fill out the form below and we will get in contact with you.

For sales enquiries, please email [email protected]. For copyright enquiries, please email [email protected].

Name*
5 + 7 = ?*
This field is for validation purposes and should be left unchanged.
1

Mungu, mtawala mwema na muumba


Jinsi Biblia inavyosema

Umestahili wewe, Bwana wetu na Mungu wetu, kuupokea utukufu na heshima na uweza; kwa kuwa wewe ndiwe uliyeviumba vitu vyote, na kwa sababu ya mapenzi yako vilikuwako, navyo vikaumbwa. (Ufunuo wa Yohana 4:11)

Msingi wa ujumbe wa Kikristo ni kwamba Mungu peke yake ndiye mtawala aliye hai na wa kweli. Mungu ndiye Bwana na Mfalme wa kila kitu kilichopo. Tofauti na watawala wengi wa kibinadamu, Mungu si fisadi wala si mwenye kujitumikia. Mungu ni mtawala mwema na mwenye upendo kabisa, akitunza ulimwengu wake na kutoa kwa ukarimu siku zote, naye huutawala ulimwengu kwa haki.

Kwa sababu Mungu aliumba kila kitu, Mungu ndiye mtawala wa kila kitu. Mungu ndiye chanzo na muumba wa yote yaliyopo, pamoja na ulimwengu mzuri ambamo tunaishi. Huu ni ulimwengu wake. Aliuumba, na anausimamia.

Pia Mungu alituumba sisi wanadamu.

Mungu alituumba sisi wanadamu na akatupa nafasi ya kipekee katika ulimwengu wake mzuri. Mungu alitupa sisi wanadamu mamlaka ya kuutawala ulimwengu, kuutunza na kuusimamia—na wakati wote kumheshimu Mungu na kumtii kama mtawala wetu, na kumshukuru kwa ukarimu wake.

Muhtasari
  • Mungu ndiye mtawala wa ulimwengu.
  • Aliumba ulimwengu.
  • Alitufanya tutawale ulimwengu wake mzuri, tukimshukuru na kumheshimu.
Hivi ndivyo Mungu alivyoumba vitu vikawa. Lakini ni wazi kwamba hivi sivyo tunavyoona ulimwengu ulivyo sasa. Nini kilitokea?
2

Uasi wetu dhidi ya Mungu


Jinsi Biblia inavyosema

Sisi sote kama kondoo tumepotea; kila mmoja wetu amegeukia njia yake mwenyewe… (Isaya 53:6a)

Chanzo cha kila kitu kibaya katika maisha yetu na katika ulimwengu ni wakati ule ambapo binadamu walichagua vibaya. Tangu mwanzo kabisa, hatukutaka Mungu kuwa mtawala wetu. Tulimkataa Mungu kabisa na tukajaribu kuishi kwa kuzifuata njia zetu wenyewe tukipingana naye.

Sisi sote tunafanya hivi katika maisha yetu. 

Muda mwingi, tunamsahau Mungu au kumweka mbali, na kuishi maisha yetu wenyewe kama hayupo. Hatumshukuru kama itupasavyo akiwa muumba wetu mkarimu atutunzaye. Hatumheshimu wala kumtii kama astahilivyo mtawala wetu. Tunafuata tamaa zetu na mambo yetu, na tunaishi jinsi tunavyoona kuwa bora sisi wenyewe.

“Dhambi” ndilo neno la Biblia kwa uasi huo dhidi ya Mungu. Biblia inasema sisi sote tunatenda dhambi—ikiwa ni watu wa dini au la.

Kwa uasi huo sisi wanadamu tumejifanya miungu wasio kweli, yaani kila mmoja amejifanya bwana juu ya maisha yake mwenyewe, akienenda kwa mapenzi yake mwenyewe. Kila mmoja hujaribu kuutumia ulimwengu na kuwatumia watu wengine kwa mapenzi na manufaa yake mwenyewe.

Haishangazi hata kuona inashindikana. Hatuwezi kujitawala na hivyo tunapata matokeo mabaya, pamoja na madhara makuu ambayo tunaleta juu yetu wenyewe, juu ya jamii, na juu ya ulimwengu.

Muhtasari
  • Sisi sote tunamkataa Mungu kuwa mtawala wetu. Tunajaribu kuishi kwa njia zetu wenyewe.
  • Kwa kuasi dhidi ya Mungu tunajiumiza wenyewe, tunawaumiza watu wengine, na pia tunauumiza ulimwengu.
Swali ni hili: Mungu atafanya nini juu ya uasi wetu dhidi yake?
3

Haki ya Mungu


Jinsi Biblia inavyosema

Na kama vile watu wanavyowekewa kufa mara moja, na baada ya kufa hukumu … (Waebrania 9:27)

Mungu ni mtawala mwema na kwa hiyo uasi wetu dhidi yake sio jambo dogo kwake. Mungu anatuwajibisha kwa matendo yetu. Maana ni muhimu kwake jinsi tuenendavyo. Ni jambo zito kwamba tumemdharau Mungu, na tumewatendea vibaya watu wengine, na tumeharibu ulimwengu wake.

Mungu hataruhusu uasi uendelee milele. Ikiwa Mungu angeacha uasi bila hukumu, ingekuwa amekosa kutenda haki.

Tunaona hukumu ya Mungu dhidi ya uasi wetu katika kifo. Mateso na kifo sio asili. Uharibifu, ubovu na kifo katika ulimwengu ni sehemu ya adhabu yetu kwa sababu tulimkataa Mungu.

Lakini kuna hukumu zaidi ambayo tutaikabili. Sisi sote tutasimama mbele za Mungu na kutoa hesabu ya maisha yetu, kwa mabaya tuliyofanya, na kwa vile tulivyomkataa Mungu mtawala wetu.

Siku ile ya hukumu, Mungu atatupatia kile tulichokitamani, yaani, kuwa mbali naye. Atatutenga naye kabisa. Kutengwa na Mungu kabisa, maana yake ni maangamizi yasiyoisha, kwa sababu Mungu ni chanzo cha uzima na vitu vyote vizuri.

Adhabu hiyo inatisha kweli. Lakini sisi sote tunakabiliana nayo maana kila mmoja tumemwasi Mungu.

Muhtasari
  • Mungu hataturuhusu kumwasi milele.
  • Kwa uasi huo, Mungu anatoa adhabu ya kifo na hukumu.
Jambo hili sio rahisi kulisikia. Maana yake ni kwamba sisi sote tuko kwenye tatizo kubwa. Lakini hukumu si mwisho wa habari za Biblia.
4

Mungu alimtuma Yesu afe kwa ajili yetu


Jinsi Biblia inavyosema

Sisi sote kama kondoo tumepotea; kila mmoja wetu amegeukia njia yake mwenyewe; na BWANA ameweka juu yake maovu yetu sisi sote. (Isaya 53:6)

Mungu anaupenda ulimwengu aliouumba, na anatupenda wote kila mmoja. Mungu hakutuacha tupate matokeo ya uasi wetu. Mungu alimtuma mwana wake mwenyewe ulimwenguni. Yesu Kristo ndiye Mwana wa Mungu, na Mungu alimtuma ili atuokoe.

Tofauti na sisi, Yesu hakuasi dhidi ya Mungu. Siku zote aliishi kwa mapenzi ya Mungu na chini ya mamlaka yake. Wakati wote Yesu alimheshimu na kumshukuru Mungu. Yesu alimtii Mungu katika kila kitu. Hakustahili hukumu ya Mungu kwa namna yoyote. Hakustahili kufa.

Lakini hakika Yesu alikufa. Ingawa Mungu alimpa Yesu mamlaka ya kuwaponya wagonjwa na hata kuwafufua wafu, lakini Yesu alikubali kuangikwa na kuuawa msalabani. Kwa nini?

Habari za kushangaza ni hizi: Yesu alikufa badala yetu, mbadala wa waasi kama sisi. Alichukua mwenyewe hukumu na adhabu ambayo tulistahili, kwa kufa msalabani kwa ajili yetu. Kifo ni adhabu ya uasi, na Yesu alikufa kifo ambacho sisi tulistahili kufa.

Hayo yote sisi hatukustahili maana tulimkataa Mungu. Bali kwa sababu ya upendo wake mkuu, Mungu alimtuma Mwanawe afe kwa ajili yetu.

Muhtasari
  • Kwa sababu ya upendo wake, Mungu alimtuma Mwanawe Yesu Kristo ulimwenguni.
  • Yesu alimtii Mungu siku zote.
  • Yesu alijitwika adhabu yetu kwa kufa badala yetu.
Lakini neno hilo si lote, bali kuna zaidi.
5

Yesu ni Mtawala aliyefufuka na Mwokozi


Jinsi Biblia inavyosema

Ahimidiwe Mungu, Baba wa Bwana wetu Yesu Kristo, ambaye kwa rehema zake nyingi alituzaa mara ya pili ili tupate tumaini lenye uzima kwa kufufuka kwake Yesu Kristo katika wafu… (1 Petro 1:3)

Mungu alikubali kifo cha Yesu kama malipo kamili kwa dhambi zetu zote, na akamfufua katika wafu. Yesu alishinda kifo. Yesu alifufuka ili awe mtawala wa ulimwengu kama ilivyokuwa kusudi la Mungu kwa wanadamu hapo mwanzoni.

Yesu alichaguliwa na Mungu kuwa mtawala wa vyote na hivyo, Mungu alimweka kuwa mhukumu wa ulimwengu. Wakati Yesu atakaporudi na siku ya hukumu itakapokuja, Yesu ndiye atakayetuhukumu kwa uasi wetu dhidi ya Mungu.

Yesu si tu mfalme na mhukumu lakini pia Yesu ni Mwokozi atuokoaye kutoka kwenye hukumu. Kwa sababu alikufa kwa niaba yetu, Yesu yuko tayari kusamehe dhambi zetu zote. Mungu alikwisha kuhukumu na kuadhibu dhambi zetu zote katika kifo cha Yesu. Na sasa tunakaribishwa kuanza upya na Mungu, sio waasi tena bali marafiki waaminifu, tukimshukuru na kumpa heshima yote.

Yesu anatukaribisha kupokea kwake uzima mpya. Katika uzima huo Mungu mwenyewe anakuja kuishi ndani yetu kwa Roho wake. Tunapata furaha ya uhusiano mpya na Mungu.

Na Yesu atakaporudi tena katika utukufu wake wote, tunaweza kuwa na uhakika kabisa kuwa tutakubaliwa kwake—sio kwa sababu tunastahili, lakini kwa sababu alichukua adhabu yetu alipokufa kwa niaba yetu.

Muhtasari
  • Mungu alimfufua Yesu katika wafu ili awe mtawala na mhukumu wa ulimwengu.
  • Yesu ameshinda kifo, sasa anatoa msamaha na uzima mpya, na atarudi katika utukufu.
Hiyo inatuacha wapi? Inatubidisha kuchagua kati ya njia mbili za kuishi.
6

Njia mbili za kuishi


Jinsi Biblia inavyosema

Amwaminiye Mwana ana uzima wa milele; asiyemwamini Mwana hataona uzima, bali ghadhabu ya Mungu inamkalia. (Yohana 3:36)

Kuna njia mbili za kuamua kuishi. Njia ya kwanza ni kuendelea kuishi katika uasi wetu dhidi ya Mungu—kumdharau Mungu na kuishi jinsi tunavyoona kuwa bora sisi wenyewe. Kweli watu wengi wanachagua njia hii na inasikitisha.

Hatimaye, kwa watu wanaochagua njia hii, Mungu atawahukumu kwa haki. Hiyo hukumu haiepukiki. Kila mmoja anayeendelea kumkataa Mungu anapata sasa katika maisha yake matokeo mabaya ya uasi ule, lakini pia anakabiliana na adhabu inayotisha, yaani kutengwa na uso wa Mungu milele.

Lakini kuna njia nyingine. Ikiwa tunamgeukia Mungu na kumwomba msamaha, tukimwamini Yesu aliyefufuka kuwa mtawala na mwokozi, basi kila kitu kinabadilika.

Kwanza, Mungu anaondoa kabisa hatia yetu. Anakubali kifo cha Yesu kuwa adhabu ya uasi wetu dhidi yake. Anatusamehe bure dhambi zetu zote kikamilifu. Anamimina Roho yake mwenyewe ndani ya mioyo yetu. Anatupa uzima mpya wa milele. Japo tutakufa, lakini tutafufuliwa na kuishi naye milele. Sisi sio waasi tena, lakini ni wa familia ya Mungu. Na sasa tunaishi chini ya mamlaka ya Yesu, Mwana wa Mungu, mtawala wetu.

Muhtasari

Kuna njia mbili tu za kuishi.

Njia yetu

  • kumkataa Mungu kuwa mtawala wetu
  • kuishi kwa njia yetu wenyewe
  • Kuharibiwa katika uasi wetu
  • Kukabiliana na kifo na hukumu

Njia mpya ya Mungu

  • Kumtii Yesu aliye mtawala wetu
  • Kutegemea kifo cha Yesu na ufufuo wake
  • Kusamehewa na Mungu
  • Kupokea uzima mpya ulio wa milele

Kwa hiyo, je, wewe wataka kuishi kwa njia gani?

Namna ya kuitikia

Ikiwa kwenye swali “wataka kuishi kwa njia gani?” wewe chaguo lako likawa “njia yetu”, basi labda hujaamini ujumbe wa Kikristo kama ilivyofundishwa katika maelezo hayo. Labda hujaamini ujumbe kwa sehemu au yote. Labda hujaamini kuwa sisi kweli ni waasi dhidi ya Mungu, au kwamba Yesu alifufuka kutoka kwa wafu.

Ikiwa ni hivyo, tafadhali fikiri kwa makini na fanya utafiti zaidi. Ni jambo la maana sana, na hatupaswi kukataa ujumbe huu bila kuwa na uhakika. Labda ni vema ukisoma mwenyewe juu ya Yesu katika Biblia—hasa vitabu vile viitwavyo Injili za Mathayo, Marko, Luka na Yohana. Labda unaweza kufanya hivyo na rafiki aliye mkristo. (Ikiwa huna Biblia, basi jaribu bible.com/sw/bible.)

Lakini, ikiwa unajua kabisa kuwa umeasi dhidi ya Mungu, na unahitaji kurudi kwake na kuanza kuishi kwa mapenzi yake, basi ni kwa namna gani unaweza kufanya hivyo?

Kuna hatua tatu rahisi, nazo ni kuongea, kutii, na kuamini

1. Ongea na Mungu

Jambo la kwanza kufanya ni kuongea na Mungu. Unaweza kukiri kwake kwamba umemwasi na unastahili adhabu, halafu na umwombe akusamehe dhambi zako zote kwa sababu Yesu alikufa kwa niaba yako. Umwombe Mungu akusaidie kuachana na uasi dhidi yake na kujitahidi kuishi chini ya mamlaka ya Bwana Yesu Kristo. Sasa, unaweza kuomba kama hivi:

Mungu Baba

Najua sistahili kuwa mbele yako. Sistahili zawadi yako ya uzima wa milele. Nimekukosea kwa kuasi dhidi yako na kukataa mapenzi yako. Najutia makosa yangu na ninasikitika. Nahitaji msamaha wako.

Asante kwa kumtuma mwanao Yesu afe kwa ajili yangu ili nisamehewe. Asante kwamba alifufuka katika wafu ili anipe uzima mpya.

Naomba unisamehe na unifanye upya, ili niweze kumtii Yesu na kumheshimu kama mtawala wangu. Amina.

2. Mtii Yesu

Baada ya kuongea na Mungu ukiungama makosa yako na kuomba msamaha (kama ile sala hapo juu) hatua ya pili inafuata. Basi ni vema kutekeleza katika maisha yako ombi la kufanywa upya. Ni muhimu kuanza upya na kumwishia Yesu Kristo kwa utii na heshima.

Inatubidi kubadilisha mambo katika sehemu zote za maisha yetu. Hivyo inabidi tabia zile za uasi kuachana nazo (kama uchoyo, hasira, ubinafsi, na kadhalika). Lakini pia kuna tabia mpya zinazompendeza Mungu unapaswa kuzichukua na kuzifanyia kazi (kama ukarimu, fadhili, upendo, na uvumilivu).

Hatua hii ya pili itaendelea kwa maisha yako yote, lakini Mungu atakuwa pamoja nawe siku zote. Mungu ataendelea kusema nawe kila unaposoma neno lake, yaani Biblia. Mungu ataendelea kukusikiliza na kukusaidia kila unapomwomba. Kwa Roho wake anayekaa ndani yako, Mungu anakufanya upya na anakuwezesha ili uishi katika njia yake. Mungu atakukutanisha pamoja na Wakristo wengine ili wakuhimize na kukutia moyo.

Hivyo hatua ya pili ni kumtii Yesu Kristo na kuanza kuishi chini ya mamlaka yake Yesu mtawala wako.

3. Mwamini Yesu

Hatua ya tatu pia inaendelea. Lazima kuendelea kuweka imani yako katika Yesu.

Kuna njia moja tu na pekee kwa mtu kupata amani kwa Mungu. Unaweza kusamehewa na kupatanishwa na Mungu kwa sababu ya Yesu tu (na kifo chake na ufufuo). Mtu anaokolewa kwa kumwamini Yesu tu. Msingi wa wokovu wote na maisha yote ni Yesu na kifo chake na ufufuo wake. Basi kama Wakristo wote, japo unataka kuishi kwa njia ya Mungu, bado utakosa na kutenda vibaya. Lakini hata hivyo msingi wa wokovu ni ule ule. Sisi sote hatuna budi siku zote kuamini na kumtegemea Yesu na kifo chake msalabani kuwa ndiyo sababu pekee ya kusamahewa.

Hatupaswi kamwe kuacha kumtegemea Yesu peke yake awe namna ambayo tumesamehewa na kupewa uzima wa milele.


Ikiwa utachukua hatua hizi, unaweza kuwa na uhakika kuwa Mungu amekusamehe makosa na dhambi zako zote na pia amekupa uzima mpya.

Lakini ikiwa bado haujamwitikia Mungu kwa njia hii, unaweza kuwa na uhakika kuwa ghadhabu ya Mungu inabaki juu yako.

Ni kama umefika njiapanda katika barabara. Kuna njia mbili tu za kuishi. Sisi sote hatuna budi kuchagua kati ya njia hizi mbili.